Kesho Ni Mwanzo wa Lake Tanganyika Business Forum
- April 14, 2026
Ni siku moja tu imebaki
kabla ya kuanza kwa tukio kubwa la kiuchumi na kibiashara – Lake Tanganyika
Business Forum litakalofanyika Kigoma, Tanzania kuanzia tarehe 15–16
Aprili 2026. Forum hii, iliyoandaliwa na TANTRADE kwa kushirikiana
na wadau wa sekta ya biashara na uwekezaji, inalenga kuibua fursa mpya,
kuimarisha ushirikiano wa kikanda, na kuonyesha nafasi ya Kigoma kama kitovu
cha biashara na lango la uchumi kuelekea nchi jirani za Kongo, Burundi na
Zambia.
Maandalizi ya forum yamekamilika
kwa kiwango cha juu, na mazingira ya Kigoma yameandaliwa kupokea wageni wa
kitaifa na kimataifa. Tukio hili litakuwa na heshima ya kipekee kwani Waziri
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, atakuwa
mgeni rasmi, akiongoza ufunguzi wa forum. Aidha, Mkurugenzi Mkuu wa
TANTRADE atakuwepo kuhakikisha uratibu na uwasilishaji wa ajenda kuu za
biashara na uwekezaji unafanyika kwa ufanisi.
Washiriki wa forum watapata nafasi
ya kujadili uwekezaji katika kilimo, viwanda, miundombinu ya usafirishaji
kupitia bandari na reli ya Kigoma, pamoja na fursa za utalii zinazotokana na
mandhari ya kipekee ya Ziwa Tanganyika. Wadhamini wakuu kama Azania Bank,
SBT, TPA na TCCIA wamejitokeza kushirikiana katika maandalizi ya forum hii,
jambo linaloonyesha mshikamano wa sekta binafsi na taasisi za umma katika
kukuza uchumi wa taifa.
Kwa kuzingatia umuhimu wa tukio
hili, Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara (TanTrade) inachukua fursa hii
kualika wadau wote kushiriki kikamilifu katika forum hii, ili kwa pamoja tuweze
kuimarisha taswira ya Kigoma na Tanzania kwa ujumla katika ramani ya biashara
ya kikanda na kimataifa.