TANZANIA YAENDELEZA USHIRIKIANO WA KIBIASHARA NA CHINA KUPITIA SERA YA BIASHARA BILA USHURU
- May 12, 2026
Dar es Salaam, 11 Mei 2026
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade),
Dkt. Latifa M. Khamis, amefanya
kikao kazi na Wafanyabiashara kutoka kampuni ya Fashion Tourism Investment
ya mji wa Yiyan, Hunan nchini China, kwa lengo la kujadili namna ya kuimarisha
na kukuza fursa za biashara kati ya Tanzania na China,
Katika kikao hicho kilichofanyika Makao Makuu ya TanTrade jijini Dar
es Salaam, TanTrade iliwasilisha kwa kina fursa mbalimbali za kibiashara
zinazopatikana nchini Tanzania, ikibainisha maeneo muhimu yenye mvuto wa
uwekezaji na biashara, hususan katika sekta za viwanda, kilimo, utalii na
huduma. Hatua hii imekusudia kutoa mwongozo wa kitaalamu kwa wadau wa biashara
wa China ili kurahisisha maamuzi ya uwekezaji na kuongeza ushirikiano wa
kibiashara.
Wafanyabiashara hao walipongeza juhudi za TanTrade chini ya uongozi wa
Dkt. Latifa M. Khamis kwa kuwapatia taarifa sahihi na za kina kuhusu mazingira
ya biashara nchini Tanzania. Walieleza kuwa hatua hiyo ni chachu ya kuimarisha
uhusiano wa kibiashara baina ya pande hizo mbili, na kwamba itarahisisha
upatikanaji wa taarifa muhimu kwa wawekezaji wa China wanaotaka kuingia katika
soko la Tanzania.
Mazungumzo haya yameelezwa kuwa sehemu ya jitihada za Serikali kupitia
TanTrade katika kuimarisha diplomasia ya uchumi na biashara, kwa kutumia
fursa ya sera ya Zero Tariff inayotolewa na China kwa bidhaa za
Tanzania. Kupitia sera hii, bidhaa za Tanzania zinapata nafasi ya kuingia
katika soko la China bila ushuru, jambo linaloongeza ushindani wa bidhaa za
Tanzania na kuimarisha mapato ya taifa.
“Tunatambua umuhimu wa kutumia fursa ya Zero Tariff kwa maslahi ya
taifa. Mazungumzo haya ni hatua ya kimkakati inayolenga kuimarisha ushirikiano
wa kibiashara na kuongeza kasi ya mauzo ya bidhaa za Tanzania katika soko la
China. Tunajenga daraja la biashara ambalo litawanufaisha wafanyabiashara wa
pande zote mbili,” alisisitiza Dkt. Latifa M. Khamis.
Kwa ujumla, kikao hiki kimeweka msingi wa ushirikiano endelevu kati ya
Tanzania na China, kikilenga kuimarisha biashara ya kimataifa, kukuza uwekezaji
na kuendeleza diplomasia ya uchumi kwa manufaa ya taifa na wadau wa sekta
binafsi.