Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania

TanTrade Fostering Business

SERIKALI YA TANZANIA YAENDELEA KUKUZA USHIRIKIANO WA BIASHARA NA CHINA KUPITIA FURSA ZA MAUZO BILA USHURU

  • May 9, 2026

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea kuthibitisha dhamira yake ya kukuza biashara na ushirikiano wa kiuchumi na China kupitia mikutano ya wadau na majukwaa ya kitaalamu yanayolenga kuongeza mauzo ya bidhaa za Tanzania katika soko la China bila ushuru.
 
Akihutubia mkutano wa wadau uliofanyika leo katika Ukumbi wa Johari Rotana, jijini Dar es Salaam, Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (MB), alisisitiza umuhimu wa kutumia fursa za ushuru nafuu ili kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kimataifa. Alieleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuongeza mauzo ya nje, kukuza ajira, na kuimarisha mapato ya taifa. Aidha, Tanzania imepanga kuanzisha dawati maalumu la kusaidia wauzaji nje wanaolenga soko la China, kama sehemu ya mageuzi mapana ya kusaidia wafanyabiashara wa ndani kunufaika na fursa zinazopanuka za biashara na China.
 
Waziri Kapinga pia aliitaka Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) kuendelea kuwaunganisha wafanyabiashara wa Tanzania na wenzao wa China, sambamba na kuhusisha wataalamu wenye ujuzi wa lugha ya Kichina ili kurahisisha mawasiliano, kuondoa vikwazo vya lugha, na kufungua zaidi fursa za biashara kwa sekta binafsi na wadau wa viwanda.
 
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TanTrade, Dkt. Latifa Khamis, alisisitiza dhamira ya taasisi hiyo ya kuendelea kuwa daraja la biashara kati ya Tanzania na masoko ya kimataifa. Alieleza kuwa TanTrade imejipanga kutoa msaada wa kitaalamu kwa wafanyabiashara wa ndani ili kuhakikisha mawasiliano na majadiliano ya kibiashara yanakuwa na ufanisi mkubwa. Dkt. Khamis aliongeza kuwa TanTrade itaendeleza majukwaa ya ushirikiano wa moja kwa moja kati ya wafanyabiashara wa Tanzania na wenzao wa China, kwa lengo la kuongeza mtiririko wa bidhaa na uwekezaji.
 
Mkutano huo ulihudhuriwa na wadau mbalimbali wa sekta ya viwanda na biashara, ambapo washiriki walipongeza juhudi za Serikali na TanTrade katika kuhakikisha bidhaa za Tanzania zinapata nafasi kubwa zaidi katika soko la China, kwa manufaa ya taifa na wananchi wake