UZINDUZI WA MAANDALIZI YA USIKU WA DHAHABU – 50 DITF,
- May 25, 2026
24 Mei 2026, Dar es Salaam
Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) imeanza rasmi maandalizi ya Usiku wa Dhahabu wa DITF (Golden Jubilee Night), tukio la
kipekee litakalofanyika tarehe 6 Julai 2026 kama sehemu ya kilele cha
maadhimisho ya Miaka 50 ya Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es
Salaam (Sabasaba). Hatua ya maandalizi ilianza rasmi kwa Sherehe ya
Maandalizi ambayo imefanyika tarehe 24 Mei 2026 Dar es Salaam,
ikihudhuriwa na wadau wa sekta ya umma na binafsi, wafanyabiashara, wawekezaji
na kampuni za kimataifa.
Mhe. Exaud Silaon Kigahe (MB), Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, ambaye alikuwa mgeni rasmi, alisisitiza kuwa
tukio hilo ni ujumbe mahsusi kwa umma kwamba kuna jambo kubwa na la kihistoria
linakuja. Alieleza kuwa Sabasaba 2026 itakuwa zaidi ya maonyesho ya
kibiashara ya kawaida; ni jukwaa la kitaifa na kikanda litakalojumuisha bidhaa,
huduma, teknolojia na ubunifu wa Watanzania, sambamba na kuimarisha nafasi ya
Tanzania katika diplomasia ya kiuchumi na ushirikiano wa kikanda.
Kwa upande wake, Dkt. Latifa M. Khamis, Mkurugenzi Mkuu wa TanTrade,
alibainisha kuwa Sabasaba ya 2026 siyo tu fahari ya Tanzania, bali ni mali
ya Watanzania wote. Alisisitiza kuwa maonyesho hayo ni alama ya mshikamano
wa kitaifa na nafasi ya Tanzania kujiweka kama kitovu cha biashara na uwekezaji
katika Afrika Mashariki na Kati. Aliwataka wananchi na wadau kujitokeza
kwa wingi kushiriki, akisisitiza kuwa ushiriki wao utakuwa mchango wa moja kwa
moja katika kukuza uchumi wa taifa na kuonyesha taswira chanya ya Tanzania
kimataifa.
“Usiku wa Dhahabu”
umebeba taswira mpya ya maonesho ya mwaka huu, ukiahidi burudani ya kiwango cha
juu, mwangaza wa kipekee, maonesho ya kisasa, kutambua wadau waliotoa mchango
mkubwa katika safari ya miaka 50, pamoja na kuunganisha sekta za biashara,
uwekezaji na ubunifu chini ya jukwaa moja. Tukio hili linatarajiwa kuwa moja ya
vivutio vikubwa ndani ya Maonesho ya Jubilei ya Dhahabu ya Sabasaba,
yatakayofanyika kuanzia tarehe 28 Juni hadi 13 Julai 2026.
Waandaaji wameeleza kuwa Usiku wa Dhahabu si burudani pekee, bali
ni ishara ya heshima kwa safari ya mafanikio ya Sabasaba tangu kuanzishwa
kwake, sambamba na kufungua ukurasa mpya wa fursa za biashara, teknolojia na
ushirikiano wa kimataifa. Wageni watakaohudhuria watapata nafasi ya kushuhudia
historia ikikutana na ubunifu wa kizazi cha sasa katika mazingira yatakayobeba
hadhi ya Jubilei ya Dhahabu.
Sherehe ya maandalizi ya tarehe 24 Mei 2026 imeweka msingi
thabiti wa maandalizi ya Usiku wa Dhahabu na maonyesho ya Sabasaba ya mwaka
huu. Ushiriki wa wadau mbalimbali, wakiwemo taasisi za umma, mashirika binafsi
na kampuni za kimataifa, umeonesha dhamira ya pamoja ya kushirikiana na
TanTrade katika kufanikisha maadhimisho haya ya kihistoria. Tukio hili
limefungua ukurasa mpya wa mshikamano wa kitaifa, ushirikiano kati ya sekta
binafsi na umma, na kuimarisha nafasi ya Tanzania katika ramani ya biashara ya
kikanda na kimataifa.