TANTRADE YAWAJENGEA UWEZO WANAFUNZI WA MASOMO YA BIASHARA NCHINI ILI WAZIJUE SHERIA, KANUNI NA TARATIBU ZA UFANYAJI BIASHARA ZILIZOWEKWA NA SERIKALI.
- August 25, 2023
.................................
Na. Norah Thomas- TanTrade Dar es salaam.
18 Agusti 2023.
Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) Leo Tarehe 18 Agusti 2023, imetoa Mafunzo kwa Wanafunzi wa kidato cha tano wa shule ya Sekondari BaoBab iliyopo jijini Dar es salaam, yenye malengo ya kujua kazi za TanTrade na kuwajengea uwezo Wanafunzi hao ili kuelewa ni kwa namna gani TanTrade inafanya kazi ili kuwasaidia Jumuiya ya Wafanyabiashara, pamoja na kufahamu miongozo mbalimbali ya Ufanyajibiashara nchini.
Mafunzo hayo yamefanyika Leo Tarehe 18 Agusti 2023 katika ukumbi wa TanTrade uliopo barabara ya Kilwa jijini Dar es salaam.
Akitoa mada katika Mafunzo hayo Afisa Biashara kutoka TanTrade Bi. Marcelina Antony amesema TanTrade ni Taasisi ya Serikali iliyopewa Mamlaka ya udhibiti, utendaji, na ushauri wa kuendeleza na kukuza biashara za ndani na nje ya Tanzania.
Hivyo Wafanyabiashara wengi wamenufaika kupitia TanTrade kwa kujengewa uwezo wa kuwezeshwa kufanya biashara kiutaalamu na kiushindani kupitia Mafunzo ya Biashara.
Pia TanTrade imefanikiwa kuwaunganisha wafanyabiashara kutoka Tanzania na wauzaji na wanunuzi kutoka nje ya nchi, na kuwasaidia Wafanyabiashara kukua kibiashara kupitia Maonesho ya biashara yanayoratibiwa na TanTrade kama vile , Maonesho ya SabaSaba pamoja na misafara mbalimbali ya biashara.
Naye Afisa Biashara kutoka TanTrade Bi. Mwanaidi Chiro ameongeza kuwa TanTrade pia inahusika na Wafanyabiashara wanaofuata sheria za nchi za Ufanyaji biashara na inaandaa Makongamano mbalimbali ya kibiashara, kwa mfano kongamano la sudani ambapo tulipata oda ya Mahindi na tulitangaza huduma zetu za afya kama vile huduma zinazotolewa na hospitali ya Muhimbili, Kwa kufanya hivyo tulitangaza bidhaa na huduma zinazozalishwa na Watanzania na kusaidia Wafanyabiashara kupata Masoko makubwa ya nje ya nchi.
Sambamba na hayo TanTrade pia ina jukumu la kuratibu misafara na Makongamano mbalimbali ya ndani na nje ya Tanzania.
"Kama kuna Waoneshaji wanatoka nje ya nchi na kuja Tanzania kuonesha bidhaa zao, wanakaguliwa kama wamekidhi vigezo na kufuata sheria za uoneshaji ikiwa ni pamoja na kuomba vibali na kukamilisha taratibu zote. hivyo Serikali inahusika na utengenezaji wa Mazingira wezeshi ya kufanya biashara, ikiwa ni pamoja na kutengeza mifumo wezeshi na rafiki ili kuhakikisha kwamba muuzaji anaweza kuuza na kununua biashara.’’ Alisema.
Aidha Afisa Biashara kutoka TanTrade Bw. Melchizedek Salingo aliongeza kuwa TanTrade inawasaidia Wafanyabiashara kwa kufanya utafiti wa Soko la ndani na Soko la nje ili kujua ni bidhaa zipi zinazohitajika sokoni ili Wafanyabiashara waweze kuzalisha na kutoa huduma inayotokana na mahitaji ya Soko husika.
Naye Mwalimu wa somo la Biashara kutoka shule ya sekondari ya BaoBab Mwl. Mtinda kengela kwa niaba ya shule ya BaoBab ametoa shukrani kwa Uongozi wa TanTrade kwa kuwapokea na kuwapa mafunzo Wanafunzi hao yatakayowajenga kibiashara.