Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania

TanTrade Fostering Business

RAIS DKT. MWINYI AFUNGA MAONESHO YA 47 YA SABASABA (47 DITF 2023)

  • July 26, 2023

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk Hussein Mwinyi amesema Maonesho ya 47 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (DITF) yameonekana kuwa  ya kuvutia na ya kipekee, kutokana na maandalizi ya hali ya juu pamoja na wingi wa ubora wa bidhaa na huduma  zinazoonyeshwa.

Kwa maboresho zaidi, aliagiza mamlaka zinazohusika kufuta minyororo ya ukiritimba isiyo ya lazima kwa biashara na uwekezaji ili kustawi na kuvutia washiriki zaidi, pia amezitaka Taasisi zinazosimamia biashara kuhakikisha zinaondoka urasimu na kuwawezesha Wafanyabiashara nchini kwa kuwawekea Mazingira rafiki ya Biashara zao.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo tarehe 13 Julai 2023, katika Uwanja wa Mwl. JK Nyerere Dar es salaam alipokuwa akifunga Maonesho ya 47 ya Biashara ya Kimataifa mahalufu kama SabaSaba  ambapo  alisema ili kupunguza gharama za kufanya biashara, kero za tozo zinapaswa kufutwa pia Serikali ya Tanzania Bara na Visiwani  zitashirikiana katika kuhamasisha ukuaji wa Biashara na Uwekezaji kwa kufanyia kazi maoni ya Wafanyabiashara nchini.

Vile vile, alishauri wazalishaji wa ndani ambao wamepokea maagizo kutoka kwa makampuni ya kigeni kuzingatia viwango vinavyohitajika.
Pia Dkt Mwinyi aliongeza kuwa  Mwaka huu, jumla ya makampuni 3,500 yakiwemo 267 kutoka nje ya nchi yalishiriki katika maonyesho hayo, hatua aliyoitaja kuwa ni mafanikio kutokana na mipango inayoendelea kutekelezwa ili kuboresha mazingira ya biashara.
Maonesho yameongozwa na Kauli Mbiu ya ‘’Tanzania ni Mahala sahihi pa Biashara na Uwekezaji’’ ikiwa inaenda sambamba na utekelezaji wa Majukumu ya TanTrade.

Akizungumza katika hafla ya ufungaji wa Maonesho hayo Mkurugenzi Mkuu wa TanTrade Bi. Latifa M. Khamis amesema kuwa  idadi ya washiriki imeongezeka kutoka washiriki 3,200 mwaka 2022 hadi kufikia washiriki 3,500 mwaka 2023, sawa na ongezeko la asilimia 9%. Kati ya hao, Washiriki wa ndani ni 3,243 ukilinganisha na 2,880 mwaka  2022 sawa na ongezeko la asilimia 18%. Kadhalika Washiriki wa nje walikuwa 267 kutoka nchi 17 zinazojumuisha, China, Ghana, India, Indonesia, Japan, Kenya, Singapore, Syria, UAE, Uturuki, Iran, Rwanda, Burundi, Uganda, Algeria, Misri, Korea, Malaysia na Pakistan.

Vilevile alisema  zaidi ya Watembeleaji 259,966 walifanikiwa kuingia katika Uwanja wa Maonesho wa Mwl. J. K. Nyerere kwa ajili ya mahitaji mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi ukilinganisha na Watembeleaji 265,957 mwaka 2022.
 ‘’Maonesho ya 47 yamefanikisha kuingia kwa jumla ya makubaliano tisa (9) ya ushirikiano (MOU) katika sekta na maeneo mbalimbali yakiwemo maeneo ya Ununuzi wa Pamba ya Tanzania tani 30,000 kwa mwaka baina Bodi ya Pamba na makampuni kutoka nchi ya Algeria, Ununuzi wa Katani ya Tanzania kati Bodi ya Katani na Makampuni kutoka nchi ya India na Ushirikiano wa Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine, Morogoro (SUA) na Chuo Kikuu cha Kilimo cha Chaudhary Charan Singh, Haryana-India kwenye maeneo mahususi ya kubadilishana wanafunzi (Exchange Programmes), mafunzo kwa njia ya mtandao (Online Programmes) na mafunzo ya kawaida (Offline Programmes) ambapo masomo yaliyopewa kipaumbele ni Kilimo (Agriculture), Biashara ya Kilimo (Agribusiness), Teknolojia kwa viumbe hai (Biotechnology), Sayansi ya Chakula (Food Science) n.k.’’ Alisema.

Aidha Bi. Latifa aliongeza kuwa, Kupitia jukwaa hili la Maonesho, Washiriki wameweza kufanya mauzo ya bidhaa na huduma yenye thamani ya shilingi milioni 3,820.70 ukilinganisha na shilingi milioni 3,592.50 Mwaka 2022. Vilevile, kupitia Mikutano ya kibiashara (B2B) iliyokutanisha Wadau kutoka sekta mbalimbali ndani na nje ya nchi, imewezesha kufanyika kwa mazungumzo na makubaliano ya kibiashara ambapo oda za bidhaa zenye thamani ya shilingi bilioni 16.98 zimepatikana. Nikuhakikishie, TanTrade itaendelea kushirikiana na wadau hawa ili kufuatilia kwa ukaribu utekelezaji wa makubaliano hayo na kuwezesha mauzo ya bidhaa hizo.

Pia alifafanua kuwa Maonesho  hayo yalifanikiwa kutoa jumla ya kazi za muda 11,687.
“Tuliweza kutoa ajira za muda katika shughuli zilizokuwa zikiendelea hapa viwanjani, ikiwa ni pamoja na kufanya usafi, usafiri, mapambo, vyakula, migahawa,” alisema Bi Latifa.