Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania

TanTrade Fostering Business

TANTRADE YAHAMASISHA USHIRIKI WA MAONESHO YA MIAKA 50 KATIKA MAADHIMISHO YA SIKU YA WAFANYAKAZI

  • May 4, 2026

TANTRADE YAHAMASISHA USHIRIKI WA MAONESHO YA MIAKA 50 KATIKA MAADHIMISHO YA SIKU YA WAFANYAKAZI

Dar es Salaam, 1 Mei 2026

Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) imeungana na wafanyakazi duniani kuadhimisha Siku ya Wafanyakazi Duniani, tukio linalotambua mchango mkubwa wa wafanyakazi katika kukuza uchumi wa taifa na ustawi wa jamii. Maadhimisho hayo yamefanyika katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam, yakihudhuriwa na viongozi wa serikali, wadau wa sekta binafsi, pamoja na wananchi kutoka makundi mbalimbali.

Katika maadhimisho hayo, TanTrade imetumia jukwaa hilo kuhamasisha wadau wa biashara kushiriki na kudhamini Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam 2026 (DITF 50 Jubilee), yanayoadhimisha Miaka 50 ya mafanikio na historia ya maonesho hayo. Maonesho haya yameendelea kuwa chachu ya maendeleo ya sekta ya biashara kwa kutoa nafasi ya kuonesha bidhaa na huduma, kukuza ubunifu, kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa, pamoja na kufungua milango ya fursa za masoko ya ndani na nje ya nchi.

Aidha, TanTrade imesisitiza kuwa wafanyakazi ni nguzo ya msingi katika kufanikisha majukumu ya taasisi hiyo, hususan katika kuratibu maonesho ya biashara, kuunganisha wafanyabiashara na fursa mbalimbali za uwekezaji, na kuendeleza ubunifu wa kitaifa. Kupitia juhudi, maarifa na ubunifu wa wafanyakazi, taasisi imeendelea kuchochea ukuaji wa sekta ya biashara, kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania kimataifa, na kuimarisha taswira ya taifa katika majukwaa ya biashara ya dunia.

TanTrade imewahimiza wadau wote serikali, sekta binafsi, na wananchi kuunga mkono maonesho haya ya kihistoria, ambayo si tu yanadhihirisha mchango wa wafanyakazi, bali pia yanajenga msingi wa uchumi imara na endelevu kwa vizazi vijavyo.